Saturday, 31 August 2013

IGP Ahamisha Maafisa wake wa Police Uwanja wa Ndege



Ndege ya Tanzania





Dar es Salaam. Siku chache baada ya kuibuliwa kwa kashfa ya kupitishwa kiholela kwa dawa za kulevya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Jeshi la Polisi limemwondoa Kamanda wa Polisi wa Viwanja vya Ndege Kamishna Msaidizi (ACP), Deusdedit Kato pamoja na Mkuu wake wa Upelelezi, David Mwafwimbo.
Mbali ya maofisa hao, pia jeshi hilo limemwondoa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Linus Sinzumwa, naye ikiwa ni miezi michache baada ya kutokea kwa ghasia wakati baadhi ya wakazi wa huko walipokuwa wakipinga mpango wa Serikali wa ujenzi wa bomba la gesi kwenda Dar es Salaam.
Nafasi ya Kamanda Sinzumwa imechukuliwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), Zelothe Stephen kutoka Makao Makuu ya Polisi.
Taarifa iliyotolewa jana na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso ilisema Mkuu wa jeshi hilo, Inspekta Jenerali (IGP), Said Mwema amemteua, ACP Selemani Hamisi kuchukua nafasi ya Kato ambaye anahamishiwa makao makuu ya jeshi hilo. Kabla ya uteuzi huo, Kamanda Hamisi alikuwa Makao Makuu Idara ya Upelelezi.
IGP Mwema pia amemteua Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Hamad Hamad kuchukua nafasi ya Mwafwimbo aliyehamishiwa mkoani Lindi kuwa Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Lindi (OCD).
Taarifa hiyo ya Polisi ilisema uhamisho huo ni wa kawaida kwa mujibu wa kanuni, taratibu na miongozo yake. Hata hivyo, katika siku za karibuni, kumekuwa na malalamiko mengi kuwa vyombo vya usalama katika uwanja huo vimeshindwa kudhibiti biashara hiyo na matokeo yake Tanzania imechafuka katika medani ya kimataifa kutokana na idadi kubwa ya vijana wake kukamatwa sehemu mbalimbali duniani.
Matukio ya karibuni yanahusisha kukamatwa kwa wasanii Agnes Masongange na Melisa Edward waliokamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo, Johannesburg, Afrika Kusini.
Kutokana na kashfa hiyo, Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe aliamua kulivalia njuga suala hilo na kuchukua hatua kadhaa na pia alifichua jinsi wasichana hao walivyosaidiwa kupitisha dawa hizo na mtandao uliohusisha polisi, maofisa usalama wa taifa na baadhi ya wafanyakazi wa JNIA.
RPC Mtwara
Sinzumwa anaondoka Mtwara baada ya ghasia kubwa zilizozuka Mei mwaka huu wakati baadhi ya wakazi wa Mtwara walipokuwa wakipinga gesi kutoka Msimbati kusafirishwa kwa bomba hadi Dar es Salaam.
Katika ghasia hizo, ambazo Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), liliingilia kati, polisi walishutumiwa na wakazi wa huko kwa kutumia nguvu kubwa na kuwasababishia madhara.

Tembo weusi wa Tanzani

KIKOSI KAZI CHA UHAMIAJI...

BARAGUMU LA MNYONGE
 
Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Kagera imeanza kampeni ya kuwahamasisha wahamiaji haramu ambapo mpaka sasa hawajaondoka nchini kurudi makwao kuomdoka mara moja kabla ya kuanza kwa zoezi la kuwaondoa kwa nguvu katika oparesheni inayotarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa.

Mfawidhi wa kitengo cha Upelelezi, Doria na Misako katika idara hiyo mkoa wa Kagera ASIS. Jeremiah Mwakibinga
Mmoja wa Maofisa uhamiaji akifuatilia kwa makini maelezo yaliyokuwa yakitolewa na ASIS. Mwakibinga wakati akiongea na viongozi na wananchi wa kijiji cha Ruhama
alisema kwamba kwa kuanza kampeni hiyo imeanza katika wilaya ya Bukoba Vijijini na baadaye itaendelea kwa wilaya zote za mkoa wa Kagera.
ASIS. Mwakibinga, ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Upelelezi Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Kagera akisikiliza swali kutoka kwa mmoja wa wananchi katika kijiji cha Ruhama alipokwenda kuhamasisha wananchi na viongozi kushirikiana na Idara hiyo kuwataka wahamiaji haramu kuondoka nchini kwa hiyari

Alisema kwamba kampeni hiyo imelenga si kwa wahamiaji pekee bali pia kwa viongozi na wananchi kwa ujumla. ''Tunajua kwamba Wahamiaji Haramu wakituona wanakimbia, mfano tulipofika katika kijiji cha Kagarama, hivyo kampeni hii tunaifanya kwa viongozi wa vijiji na wananchi pia. Tumeongea na wananchi
Kikosi cha Upelelezi chini ya Kamanda Mwakibinga wakiongea na Afisa Mtendaji wa kijiji cha Katerero
katika vijiji vya Kibirizi, Rugazi, Kagarama, Masheshe na Katoro kwamba wao washirikiane nasi kwa kuwakataa wahamiaji haramu kwani wanajua na wanaishi nao siku zote, kuwakataa manake kuwaeleza ukweli kwamba warudi kwao, pia wananchi wawashinikize viongozi wao kuwaondoa wahamiaji haramu. Kwa upande wa viongozi wa vijiji na kata, tumewasisitiza kwamba wafanye juhudi katika kuwahimiza wahamiaji hawa waondoke, na kama mtu kaambiwa aondoke halafu amekataa basi walete taarifa ofisini kwetu siye tutamshughulikia.'' Alieleza Mwakibinga.

Wahamiaji haramu kutoka nchi za Rwanda, Burundi na Uganda ambao wapo katika mkoa wa Kagera inasemekana waliondoka na sasa wameanza kurejea tena nchini baada ya kuona kuwa Oparesheni aliyosema Raisi wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dokta Jakaya Mrisho Kikwete ya
Maafisa Uhamiaji wakiranda mitaani katika kijiji cha Masheshe wilaya ya Bukoba Vijijini
kuwaondoa kwa nguvu wahamiaji haramu baada ya wiki mbili haifanyiki, wengi wamerudi wakidai ile ilikuwa ni 'danganya toto' tu hakuna oparesheni itakayokuja.



 


Wananchi wa kijiji cha Kibirizi wakimsikiliza Kamanda wa Upelelezi Uhamiaji mkoa Kagera wakati alipokuwa akiongea nao kuhusu suala la wahamiaji haramu mkoa wa Kagera

Sunday, 25 August 2013

CCM yawawashia moto Kagasheki, Amani

 
Tanzania




Dodoma. Wakati Kamati Kuu ya CCM imeamua kuumaliza mgogoro wa madiwani wake wa Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera kwa kutoa onyo kwa viongozi wake, ndani ya Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM), hakujatulia kwani kuna mpango wa kumwondoa Katibu Mkuu wake, Martin Shigela.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya vikao vya Kamati Kuu zimesema kwamba viongozi kadhaa wa chama hicho akiwamo Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamisi Kagasheki na Meya wa Manispaa ya Bukoba, Anatory Amani wameonywa kutokana na mgogoro wa muda mrefu katika wilaya hiyo.
Wengine waliotakiwa kupewa karipio ni pamoja na  Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kagera, Costancia Buhiye na Katibu wake, Averin Mushi ambao walitarajiwa kuhojiwa jana usiku.
Habari kutoka ndani ya vikao hivyo vinavyofanyika Mjini Dodoma zilisema hata ule uamuzi wa kuwazuia Amani na Kagasheki kufanya siasa umeonekana unaweza kuleta athari kwao na kwa chama chenyewe, hivyo kuamua kutoa onyo na madiwani waliokuwa wamefukuzwa uanachama kuachwa kuendelea na nyadhifa zao. Vyanzo hivyo vya habari vilieleza kuwa suala hilo lilikuwa tayari limeamuliwa, isipokuwa ilikuwa ni lazima wahusika waitwe kufahamishwa uamuzi dhidi yao badala ya kusikia kwenye vyombo vya habari.
Hata hivyo, hadi jana wakati tunakwenda mitamboni ni viongozi wawili tu, waliokuwa wamehojiwa na Kamati Kuu ambao ni Buhiye na Mushi kwa kuwa tayari walikuwapo Dodoma wakiwa ni wajumbe wa Halmashauri Kuu.
Balozi Kagasheki na Amani licha ya kwamba walikuwa wamewasili hapa, suala lao liliahirishwa kutangazwa kuwasubiri Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Bukoba Mjini, Yussuf Ngaiza na Katibu wa CCM Wilaya hiyo, Janeth Kayanda waliochelewa kufika mjini hapa baada ya gari lao kuharibika.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema uamuzi wa Kamati Kuu ungetolewa baada ya kumalizika kwa hatua ya kuwahoji viongozi hao jana.
Mgogoro wa Manispaa hiyo unatokana na miradi iliyopangwa na Meya Amani, ambayo inapingwa na baadhi ya madiwani wa CCM wa Manispaa akiwamo Balozi Kagasheki, ambaye pia ni Waziri wa Maliasili na Utalii.
Mbunge wa Bukoba
Hali ya siasa mkoani humo ilichafuka zaidi baada ya  Halmashauri ya CCM ya Mkoa wa Kagera kuwafukuza madiwani wanane kwa kosa la kumpinga Meya huyo na kupanga kumng’oa madarakani.
Madiwani hao ni Richard Gaspar (Miembeni), Murungi Kichwabuta (Viti maalumu), Alexander Ngalinda ambaye pia ni Naibu Meya (Buhembe) na Deusdedit Mutakyahwa (Nyanga), Robert Katunzi (Hamugembe), Samwel Ruhangisa (Kitendaguro), Dauda Kalumuna (Ijuganyondo) na Ngaiza(Kashai).
Hata hivyo, uamuzi huo wa kuwafukuzwa ulisimamishwa na Sekretarieti ya CCM ambayo ilisema kuwa Kamati Kuu ndiyo iliyokuwa na madaraka ya kutoa uamuzi wa mwisho dhidi yao na kuwataka kuendelea na kazi wakisubiri hatima yao.

Katika hatua nyingine, kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), ambacho kilikuwa kimalizike jana kimeongezewa siku moja zaidi na kitafungwa rasmi leo.


Nape alisema hatua hiyo imechukuliwa ili kuwapa nafasi wajumbe wake kuipitia Rasimu ya Katiba.
UVCCM kwawaka moto
Baraza Kuu la UVCCM linakutana mjini Dodoma wiki hii pamoja na mambo mengine ni kupitisha jina la Katibu Mkuu mpya wa umoja huo.
Uteuzi huo unafanywa na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana, Sadifa Juma Khamis, ambaye inaelezwa kuwa ameamua kumwondoa Martine Shigela.
Habari za ndani kutoka katika umoja huo, zinasema mbali na muda wa Shigela kumalizika, kumekuwapo na mgogoro ndani ya UVCCM, baina yake na Sadifa tangu alipochaguliwa mwaka jana.
Habari hizo zinasema majina matatu yamependekezwa kwa nafasi hiyo, akiwamo Katibu wa CCM Mkoa wa Morogoro, Sixtus Mapunda anayepewa nafasi kubwa. Wengine wanaotajwa kupendekezwa na Mwenyekiti na kusubiri baraka za Baraza Kuu ni wakuu wa Wilaya wawili, Elibariki Kingu (Igunga) na Anthony Mtaka (Mvomero).
Kutokana na unyeti wa nafasi ya Katibu Mkuu wa UVCCM, jana makundi ya umoja wa vijana yalikuwa yameanza kujikusanya mjini hapa kujadili, huku baadhi yakichambua ama kwa kuafiki au kupinga majina hayo.
Kuna taarifa kuwa uamuzi uliochukuliwa ni mwendelezo wa mvutano wa makundi ya wagombea urais kupitia CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Alipoulizwa jana kuhusu suala hilo, Sadifa alikataa kulizungumzia kwa undani akisema lisubiri vikao vimalizike.
“Kwanza vikao havijajadili jina la mtu anayefaa kuwa katibu mkuu, siwezi kulizungumzia. Subiri vikao vikimalizika nitakuwa tayari kuzungumza,” alisema Sadifa.

Mawindo ..Swala kukaangoni

Saturday, 24 August 2013

WATANZANIA NI LAZIMA TUFUATE SHERUA....(Haki za binadamu)




Nyonge nyongeni haki yake mpeni


Mauaji ya watu yanayofanywa na mamlaka za serikali pasipo kufuata sheria pamoja na vurugu zinazohusiana na makundi na uchawi vimegharimu maisha ya mamia ya Watanzania katika kipindi cha kwanza cha 2013, kwa mujibu wa ripoti ya hivi karibuni ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) jijini Dar es Salaam.
  • Josephine Slaa, mke wa mpiga kampeni dhidi ya rushwa na mgombea urais William Slaa, anasaidiwa kuingia katika gari la polisi baada ya kupigwa na polisi waliokuwa wakipambana na ghasia wakati wa maandamano ya chama cha upinzani tarehe 5 Januari, 2011. Ripoti mpya iliyotolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu imesema mapambano baina ya raia na vikosi vya usalama vya taifa yamesababisha raia 22 na maofisa polisi 8 kufariki dunia katika nusu ya kwanza ya 2013. [Stringer/AFP]
Wakati baadhi ya viashirio vinaonyesha kuboreka kwa kiasi ikilinganishwa na miezi sita ya kwanza mwaka uliopita, matokeo ya jumla ya kituo hicho yameibua wasiwasi kwamba Watanzania wanajichukulia sheria mikononi na kupuuza sheria iliyopo.
Vurugu za vikundi zilisababisha mauaji ya watu 597 katika kipindi cha nusu ya kwanza ya mwaka huu, ikiwa ni ongezeko kutoka vifo 563 kati ya Januari na Juni 2012, LHRC ilisema katika taarifa yake ya nusu mwaka iliyotolewa tarehe 29 Julai. Watu wengi kadri ya 303 waliuawa katika vurugu zilizohusiana na uchawi katika kipindi cha miezi sita ya kwanza ya 2013, ikipungua kutoka 336 katika kipindi kama hicho cha mwaka uliopita.
Katika vurugu za kuua ambazo zilitokea kipindi cha miezi sita ya mwanzo ya mwaka huu, polisi wa Tanzania, wanamgambo na vikosi vya jeshi waliwaua raia 22, ambapo raia waliwaua polisi wanane wakiwa kazini, LHRC iliripoti.
"Mwaka uliopita, watu 31 waliuawa katika mauaji yaliyofanywa na vyombo vya serikali pasipo kuzingatia sheria mwaka mzima" Mwansheria na mtafiti wa LHRC Pasience Mlowe aliiambia Sabahi. "Miezi sita ya mwaka huu, tayari watu 22 wameshauawa. Kiwango kinaidaiwa kuongezeka."
Ripoti hiyo ilionyesha ongezeko la mauaji kutokana na fikra za haki za makundi, ulinzi hafifu wa haki za raia,ukiukaji wa uhuru wa kukusanyika, na kukosa taarifa, ni miongoni mwa mambo mengi.
Mlowe alisema kwamba LHRC ilikusanya idadi kwa ajili ya ripoti yake kutoka polisi, wanaharakati wa haki za binadamu na vyanzo vingine rasmi. Hivi vinajumuisha ripoti za makamishina wa wilaya ambazo LHRC ilitumia kubainisha majina ya waathirika na kupata ukweli wa msingi kuhusu mauaji.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Watanzania wanapambana na polisi wakati wanapohisi kwamba haki zao zinakiukwa, jambo linalosababisha hali hiyo kuongezeka kwa haraka na kusababisha mauaji.
Kama mfano, ripoti ilinukuu mauaji ya tarehe 11 Januari ya maofisa wawili wa polisi kwa kupambana na ghasia za madereva wa pikipiki, zinazojulikana kama boda boda, katika wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma. Maofisa hao waliuawa katika ulipizaji kisasi kwa polisi kurusha mabomu ya machozi katika msongamano wa waandamanaji tarehe 9 Februari.
Kwa kuongezea, ripoti inasema, wahalifu wa siku zote hawawatambui maofisa wa polisi kama mawakala wa utekelezaji wa sheria na wanajibu kwa vurugu kubwa wanapokabiliwa. Kwa hiyo, kutumia udhibiti zaidi, maofisa wa polisi wanatumia nguvu za ziada wakati wa kukabiliana na umma, kwa mujibu wa ripoti.
Pia imetaja mapigano kati ya madereva wa boda boda na polisi katika mkoa wa Mtwara mwishoni mwa Januari ambayo yalisababisha vifo vya raia. Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya nchini, vurugu zilianza wakati madereva walipopinga kukamatwa kwa dereva mwenzao wa boda boda na kuingia mitaani kupinga.
"Hatua ya waendesha boda boda ilikuwa kufanya fujo, zikisababisha uharibifu mkubwa ambapo majengo ya umma,mali za CCM [Chama Cha Mapinduzi] na zile za viongozi wao zilichomwa moto," ripoti hiyo ilisema. "Katika kuchukua hatua, polisi walitumia nguvu kupita kupambana na wafanya fujo na kusababisha vifo vya watu tisa na 11 kujeruhiwa vibaya."

Suala la uchawi linazidi kuongezeka

Ripoti iligundua kwamba idadi ya vifo kuhusiana na uchawi inaendelea kuongezeka nchini Tanzania, hususani mkoani Shinyanga.
Pamoja na vifo 303 vinavyohusiana na uchawi katika nusu ya kwanza ya mwaka huu, tatizo linaongezeka kufikia viwango vya mwaka 2012, wakati watu 630 walipouawa. Waathirika waliuawa kutokana na tuhuma kutoka kwa wanajamii wenzao kwamba wamewaroga watu.
Sheria ya Uchawi Tanzania, ambayo inakataza kitendo hicho, inaueleza uchawi kama "ushirikina, urozi, kufanya uchawi, matumizi ya vifaa vya kichawi, tendo la kukusudia la nguvu zozote za kiini macho na kukusudia kumiliki maarifa yoyote ya kiini macho."
Ripoti inadhania kuwepo kwa uchawi katika mgongano wa maslahi ya kiuchumi kati ya familia zilizo jirani, hususani katika kanda ya ziwa.
"Watu wanarogana wenyewe kwa wenyewe ili kudhibitiutajiri wa familia [au ukoo]," ripoti ilisema. "[Pia] kiwango kikubwa cha wasiosoma na imani za kishirikina na kuwatumia waganga wa kienyeji [inachangia katika mauaji]."
Ripoti inasema ukosefu wa huduma za msingi za matibabu kunachochea mamlaka na imani ya watu kwa waganga wa kienyeji.
Mwanasheria na mjumbe wa timu ya utendaji ya LHRC Imelda Lulu Urrio alisema ukimya wa serikali katika masuala hayo ulikuwa unasaidia kuchochea imani za kishirikina na kuwahamasisha wakosaji kufanya mauaji haramu.
"Kama haitazuiliwa mapema, inaweza kuishia kusababisha mauaji ya watu wengi na kusababisha mauaji ya kimbari," aliiambia Sabahi.
Mwanasheria Harold Sungusiya, ambaye anaongoza programu ya utetezi na mabadiliko ya LHRC, alisema serikali inapaswa kushughulikia uchawi na mauaji yanayohusiana na uchawi, vinginevyo itasababisha machafuko nchini.
"Mtu yeyote anayechukua sheria mkononi kwa kuwaua watu walioshutumiwa anavunja sheria," Sungusiya aliiambia Sabahi. "Ndiyo, wananchi wanaweza kuwa na imani ya msingi kwamba uchawi unafanyika lakini wanapaswa kuwa na imani katika mfumo wa sheria."
Sheikh Ali Mohamed Hemed, imam wa Msikiti wa Kisiwani huko Dar es Salaam, alisema viongozi wa dini wanapaswa kuwajibika kwa kiasi kikubwa katika kuuelimisha umma.
"Quran na Biblia zinawakataza kuwaua binadamu wenzenu," aliiambia Sabahi. "Tunapaswa kufanya zaidi kama watumishi wa dini kuwaongoa wafuasi zaidi kama njia ya kuistarabisha jamii yetu."
Mchungaji Kamala Simon wa Kanisa la Kilutheri huko Dar es Salaam alisema chanzo cha tatizo kilikuwa kuharibika kwa maadili.
"Tumepoteza mwelekeo wa imani, hivyo watu hawathamini maisha tena," alisema Simon. "Kama viongozi wa dini tunapaswa kufanya [jitihada] zaidi kuirejesha nchi tulikotoka. Tunastahili amani bila ya vurugu."

Watanzania lazima wazingatie sheria

Kikundi cha utetezi wa haki za binadamu kilipendekeza kwamba wananchi wafuate sheria na kuheshimu mamlaka yaliyotolewa kwa polisi kama wasimamizi wa sheria. Iliagizwa kwa mashirika ya kusimamia sheria kuheshimu haki za binadamu na kutumia nguvu zinazotakiwa pale zinapohitajika. LHRC pia waliomba serikali iingilie kati haraka kesi zinazohusu uchawi.
Mbunge Ismail Aden Rage aliiambia Sabahi mzizi wa vurugu ulikuwa ni ukosefu wa uelewa wa jinsi kila mwananchi anavyotimiza wajibu katika kulinda haki za binadamu na uhuru wa wananchi.
Kwa mfano wakati wa maandamano, ni wananchi gani wanaweza kufanya kwa haki, sheria za kushiriki zinapaswa kufuatwa ili kuhakikisha usalama wa vyama vyote, alisema.
"Watu wetu sasa wanaandamana dhidi ya hospitali, Benki Kuu na wakati mwingine ikulu," alisema Rage. "Viongozi wetu wa kisiasa wana wajibu wa kuwaelimisha wanachama wao [kutoyakabili] mashirika yetu ya kusimamia sheria."
Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Ndani Emmanuel Nchimbi alisema serikali imepokea ripoti ya LHRC na kwamba baada ya upitiaji wa kina itatoa mpango wa utekelezaji kuhakikisha kwamba sheria na haki za wananchi zimezingatiwa na kulindwa.
"Kitu cha msingi ni utawala wa sheria," Nchimbi aliiambia Sabahi. "Watu wote wanapaswa kufuata sheria ya nchi, na hakutakuwa na mauaji kama hayo. Kama serikali tutahakikisha kwamba hili linatekelezwa."