Friday, 2 August 2013

Pasipo ‘Haki Ardhi’ amani itatoweka


  Pasipo ‘Haki Ardhi’ amani itatoweka


Baragumu

Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Udasa), juzi iliandaa kongamano ambalo mada yake kuu ilikuwa Mustakabali wa Amani na Usalama wa Wananchi Tanzania Miaka 50 Ijayo. Kongamano hilo lilikuwa la kusisimua kutokana na washiriki wengi kuchangia mada hiyo kwa hisia kali, huku wakielekeza lawama nyingi kwa Serikali kwamba inatumia Jeshi la Polisi kupora haki za raia, ikiwa ni pamoja na kukandamiza vyama vya upinzani.
Wachangiaji wengi walisema amani katika nchi yetu katika miaka 50 ijayo iko shakani kutokana na kutokuwapo kwa demokrasia ya kweli, hali ambayo walisema inaweza kusababisha vita huko tuendako. Jambo la kushangaza ni kwamba wachangiaji karibu wote waliona masuala yenye sura ya kisiasa kama ndio yatakuwa chanzo cha uvunjifu wa amani hapa nchini katika miaka 50 ijayo.
Suala la ardhi halikuzungumzwa, ingawa ndilo suala kubwa zaidi ya mengine linaloweza kuingiza nchi yetu katika machafuko iwapo masuala ya umiliki ardhi, kero na migogoro inayohusu ardhi haitapata suluhisho. Suala la ardhi limekuwa likipuuzwa na Serikali na Bunge pasipo kujua kwamba ardhi ndiyo itakayoamua hatima ya nchi yetu. Hii ni kutokana na ukweli kwamba ardhi ni rasilimali ya msingi katika uzalishaji. Hivyo, haki ya kumiliki ardhi ni njia ya kuhakikisha kuwapo kwa usalama na amani katika jamii.
Pamoja na suala la umiliki wa ardhi kuingizwa katika Katiba, bado kuna changamoto nyingi katika sekta ya ardhi ambazo zimeleta malalamiko mengi. Hizi ni pamoja na migogoro ya ardhi, kuchukua ardhi ya wananchi bila ridhaa yao na kulipa fidia ndogo isiyoendana na thamani ya ardhi.
Limejitokeza tatizo la wanasiasa kuwapora wananchi ardhi. Takwimu zinaonyesha kwamba asilimia ya kaya zenye hatimiliki ya ardhi ni ndogo na inaendelea kushuka, wakati kesi zinazohusiana na migogoro ya ardhi zinaongezeka. Kulingana na Sensa ya Utafiti wa Kilimo (ACS) ya mwaka 2007/2008, idadi ya kaya za vijijini zinazomiliki ardhi kwa kutumia hati rasmi imeshuka kutoka asilimia 7.1 mwaka 2002/2003 hadi asilimia 5.8 mwaka 2007/2008.
Takwimu za Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi zinaonyesha kuwa, idadi ya migogoro ya ardhi ambayo kesi zake zimefunguliwa imeongezeka kutoka 1,490 mwaka 2004/5 hadi 40,088 mwaka 2011, ikiwa ni ongezeko la asilimia 2,590. Hii sio ishara njema kwa mustakabali wa nchi yetu, kwani kuporwa kwa ardhi kunakofanywa na wanasiasa na vigogo serikalini ni jambo la hatari kwa amani yetu.
Hivyo, lazima Serikali isiyafumbie macho madhara ya kuchukuliwa kwa maeneo makubwa yaliyosababisha kushuka kwa umiliki wa ardhi miongoni mwa kaya za vijijini na kuongezeka kwa kesi za migogoro ya ardhi. Pia suala la kulipa fidia stahiki na kwa haraka kwa ardhi iliyonyakuliwa ni suala linalohitaji kufanyiwa kazi hivi sasa. Inashangaza kuona kuwa, pamoja na Katiba na sheria za nchi kutaka fidia ya haki na haraka, mamlaka husika zimekosa utashi na hivyo matakwa hayo hayatekelezwi.
Utashi wa kisiasa ndani ya Serikali na Bunge unahitajika katika kutekeleza matakwa ya ‘Haki Ardhi’. Vinginevyo, nchi yetu itaingia kwenye vita ya wenyewe kwa wenyewe huko tuendako, kwani historia imeonyesha kwamba hakuna mwananchi anayekubali kufa njaa kwa kukosa ardhi, huku wengine wakiwa wamejilimbikizia ardhi kubwa wasiyoihitaji.

No comments:

Post a Comment