Thursday, 15 August 2013

Spika asiwagwaye wabunge walarushwa




Spika asiwagwaye

  wabunge walarushwa







Spika wa Bunge, Anne Makinda kwa mara ya kwanza tangu achaguliwe kuliongoza
Bunge la Kumi baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2010 amekiri kwamba kuna tatizo kubwa la rushwa miongoni mwa wabunge na amezitaka Kamati za Kudumu za mhimili huyo wa dola kufanya kazi kwa uadilifu pia kuwataka wabunge kuacha vitendo vya kudai na kupokea rushwa.
Spika Makinda alitoa kauli hiyo mwanzoni mwa wiki mjini Bagamoyo, mkoani Pwani alipokuwa akifungua mafunzo ya wajumbe wa Kamati za Hesabu za Serikali Kuu (PAC), Serikali za Mitaa (LAAC) na Bajeti ambayo yaliandaliwa na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Tofauti na wakati wowote katika kipindi cha uongozi wake wa chombo hicho cha kutunga sheria, mara hii Spika Makinda alipata ujasiri na kusema wabunge wakome kuomba na kupokea rushwa, huku akionya kwamba iwapo watashindwa kuwa waadilifu wataiuza nchi.
Kwa tafsiri yoyote ile, kauli ya Spika Makinda ni nzito na ni bahati mbaya kwamba aliitoa katika mkusanyiko wa wabunge wachache badala ya kikao cha Bunge zima.
Tunasema hivyo kwa sababu inaweza ikatafsiriwa kwa makosa kwamba Spika alikuwa akiwalenga tu wabunge wa Kamati hizo tatu za Bunge wakati ukweli ni kwamba alikuwa akielekeza fadhaa zake kwa wabunge wote wa Bunge la Kumi ambalo yeye ndio kiongozi.
Pengine jambo ambalo hakulitilia maanani ni kwamba ujumbe wake ungekuwa na uzito zaidi iwapo angeutoa katika kikao mwafaka cha kuzungumzia rushwa katika Bunge ambacho kingehudhuriwa na wabunge wote. Bila shaka kikao hicho kingewapa wabunge wote fursa ya kujikosoa na hatimaye kuondoka na msimamo wa pamoja dhidi ya wabunge walarushwa.
Wapo watu wanaosema kwamba kauli ya Spika Makinda imetolewa ikiwa imechelewa na kuhoji alikuwa wapi muda wote huo hadi akaitoa wakati Bunge la Kumi likikaribia kumaliza muda wake. Hoja yao kuu ni kwamba samaki mkunje angali mbichi na wanamlinganisha Spika na mtu anayetafuta shuka kujifunika kukiwa kumekucha. Wakosoaji wanawaona wabunge walarushwa katika Bunge hili kama watu walioharibika kiasi cha kutorekebika kwa kuwa Bunge hilo liko katika kipindi cha lala salama.
Hoja za wakosoaji wa Spika kwa kweli ni za msingi. Wanasema katika uongozi wake, Spika Makinda alipata fursa tele za kutokomeza vitendo vya rushwa, lakini alishindwa kuzitumia. Alizima sauti za wabunge waliokuwa wakilalamikia vitendo vya rushwa vya baadhi ya wabunge. Ndio maana ni vigumu kumsahau Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila alipolieleza Bunge Juni 13, 2011 namna wabunge wa Kamati ya LAAC walivyokuwa wakipokea rushwa kutoka kwa watumishi wa Serikali, huku akiwataja kwa majina baadhi ya wabunge aliodai aliwakamata ‘live’ wakiwa wanafanya hivyo.
Pamoja na kumkabidhi Spika ushahidi wa tukio hilo, hadi sasa kiongozi huyo hajachukua hatua yoyote. Baada ya muda mfupi mmoja wa wajumbe wa Kamati hiyo ambaye pia alitajwa na Kafulila alikamatwa akidaiwa kupokea rushwa katika tukio tofauti na kufunguliwa kesi ambayo bado iko mahakamani.
Madai hayo ni mbali na madai ya rushwa dhidi ya wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo Spika aliivunja lakini pia akashindwa kuchukua hatua.

No comments:

Post a Comment